Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Ezekieli sura ya 37 inazungumuzia vitiji (vipande vya muti) viwili vyenye viligeuka kuwa kipande kimoja. Maana yake nini?

Kupitia nabii wake Ezekieli, Yehova alitabiri kama watu wake wangerudia katika Inchi ya Ahadi na kama wangeungana na kuwa tena taifa moja. Unabii huo ulitabiri pia kama wale wenye kumuabudu Mungu katika siku za mwisho wangeungana na kuwa taifa moja.

Yehova alimuambia nabii wake Ezekieli aandike kwenye vipande viwili vya muti. Kwenye kipande kimoja cha muti alipaswa kuandika, “Kwa Yuda na kwa wenzake, wana wa Israeli,” na kwenye kipande kingine, “Kwa Yosefu, kijiti cha Efraimu, na wenzake.” Vipande hivyo vya muti vingegeuka na kuwa kipande “kimoja tu” katika mikono ya Ezekieli.—Ezekieli 37:15-17.

Neno “Efraimu” maana yake nini? Kabila la Efraimu ndilo lilikuwa kabila lenye lilijulikana zaidi kati ya makabila kumi ya ufalme wa kaskazini wa Israeli. Kwa kweli, Yeroboamu, mufalme wa kwanza wa ufalme huo, alikuwa wa kabila la Efraimu. (Kumbukumbu la Torati 33:13, 17; 1 Wafalme 11:26) Kabila hilo lilitokana na Efraimu, mwana wa Yosefu. (Hesabu 1:32, 33) Yosefu alikuwa amepata baraka ya pekee kutoka kwa baba yake, Yakobo. Kwa hiyo, lilikuwa jambo lenye kufaa kwamba “kijiti cha Efraimu” kilifananisha makabila kumi ya ufalme wa kaskazini. Katika mwaka wa 740 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, miaka mingi mbele Ezekieli atabiri, Waashuru walipata ushindi juu ya ufalme wa kaskazini wa Israeli na wakapeleka watu katika utumwa. (2 Wafalme 17:6) Kisha miaka fulani, Wababiloni walipata ushindi juu ya Waashuru. Kwa hiyo, wakati Ezekieli aliandika unabii huo juu ya vipande vya muti, wengi kati ya Waisraeli hao walikuwa wanasambaa katika Utawala wote wa Babiloni.

Katika mwaka wa 607 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Wababiloni walipata ushindi juu ya ufalme wa kusini wa Yuda wa makabila mbili na wakapeleka watu Babiloni. Inawezekana walipeleka wengine wote wenye walibakia katika ufalme wa kaskazini wa Israeli. Wafalme wa ufalme wa kusini walikuwa wa kabila la Yuda. Makuhani pia waliishi katika Yuda kwa sababu walikuwa wanatumika katika hekalu la Yerusalemu. (2 Mambo ya Nyakati 11:13, 14; 34:30) Kwa hiyo, ilifaa kusema kama kipande cha muti “kwa Yuda” kilifananisha makabila mbili ya ufalme wa kusini.

Vipande hivyo viwili vya muti viliunganishwa wakati gani? Jambo hilo lilitokea katika mwaka wa 537 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, wakati watu fulani wa ufalme wa kusini na watu fulani wa ufalme wa kaskazini walitoka katika utumwa na kurudia Yerusalemu ili kujenga upya hekalu. Taifa la Israeli halikukuwa tena lenye kugawanyika. Tena, Waisraeli walimuabudu Yehova pamoja. (Ezekieli 37:21, 22) Nabii Isaya na Yeremia walitabiri pia umoja huo.—Isaya 11:12, 13; Yeremia 31:1, 6, 31.

Ezekieli alitabiri nini juu ya ibada safi? Alitabiri kama Yehova atafanya wale wote wenye kumuabudu ‘kuwa mumoja.’ (Ezekieli 37:18, 19) Unabii huo ulitimia katika siku zetu? Ndiyo. Unabii huo ulianza kutimia katika mwaka wa 1919. Mbele ya hapo, Shetani alikuwa amejikaza kugawanya watu wa Mungu sikuzote. Lakini katika mwaka wa 1919, watu hao walipangwa tena hatua kwa hatua na kuunganishwa tena pamoja.

Wakati huo, wengi kati ya watu wa Mungu walikuwa na tumaini la kuwa wafalme na makuhani mbinguni pamoja na Yesu. (Ufunuo 20:6) Walikuwa kama kipande cha muti kwa Yuda. Lakini, kulikuwa watu kidogo wenye walikuwa na tumaini la kuishi milele duniani. Kadiri wakati uliendelea kupita, hesabu ya wale wenye kuwa na tumaini hilo iliongezeka. (Zekaria 8:23) Walikuwa kama kipande cha muti kwa Yosefu.

Leo, watu wa vikundi hivyo viwili wanamutumikia Yehova pamoja na wako na Mufalme mumoja, Yesu Kristo. Katika unabii wa Ezekieli, anaitwa ‘mutumishi wangu Daudi.’ (Ezekieli 37:24, 25) Juu ya wanafunzi wake, Yesu alisali kwa Baba yake hivi: ‘Wapate [wao wote] kuwa kitu kimoja, kama vile ambavyo wewe, Baba, umo [uko] katika muungano pamoja na mimi na mimi nimo [niko] katika muungano pamoja na wewe.’ * (Soma maelezo ya chini.) (Yohana 17:20, 21) Yesu pia alitabiri kama kundi ndogo la watiwa-mafuta ‘wangekuwa kundi moja’ pamoja na “kondoo wengine” wake. Wote wangefuata ‘muchungaji mumoja.’ (Yohana 10:16) Kama vile Yesu alieleza, leo watu wa Mungu wote wanaishi katika umoja, iwe wako na tumaini la kuishi milele mbinguni ao duniani!

^ fu. 10 Wakati Yesu alizungumuzia ishara ya siku za mwisho, alitolea wanafunzi wake mifano mingi. Inapendeza kuona kama katika mufano wa kwanza alizungumuzia ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara,’ kikundi kidogo cha ndugu watiwa-mafuta wenye wangeongoza watu wa Mungu. (Mathayo 24:45-47) Kisha katika mifano mingine yenye alitoa, alizungumuzia watiwa-mafuta wote. (Mathayo 25:1-30) Mwishowe alizungumuzia wale wenye wangesaidia ndugu za Kristo na kuishi milele duniani. (Mathayo 25:31-46) Vilevile, wakati unabii wa Ezekieli ulianza kutimia wakati wetu, ulihusu kwanza wale wenye walikuwa na tumaini la kuishi mbinguni. Na makabila kumi ya Israeli hayafananishe kila mara wale wenye wataishi milele duniani, lakini umoja wenye kuzungumuziwa katika unabii huo unatukumbusha umoja wenye kuwa kati yao na watiwa-mafuta.