Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Ni mapendeleo na madaraka gani yaliyotokana na haki ya kuwa mwana mzaliwa wa kwanza?

Tangu nyakati za wazee wa ukoo, watumishi wa Mungu walimpa haki za pekee mtu ambaye alikuwa mwana mzaliwa wa kwanza. Baada ya kifo cha baba, mwana wake mzaliwa wa kwanza alichukua madaraka ya kichwa cha familia. Mwana huyo angeitunza familia na kuwa na mamlaka juu ya washiriki wengine wa familia ambao waliendelea kuishi nyumbani. Mzaliwa wa kwanza aliwakilisha pia familia mbele za Mungu. Ingawa wana wote walipokea urithi, mzaliwa wa kwanza alipokea urithi mkubwa zaidi. Mzaliwa wa kwanza alipokea mara mbili ya kiasi ambacho wana wengine huenda walirithi.

Katika siku za wazee wa ukoo, mwana mzaliwa wa kwanza angeweza kupoteza haki yake ya kuwa mzaliwa wa kwanza. Kwa mfano, Esau aliuza haki yake ya mzaliwa wa kwanza kwa ndugu yake mdogo. (Mwanzo 25:30-34) Yakobo alichukua haki ya mzaliwa wa kwanza ya mwana wake Rubeni, na kumpa Yosefu haki hiyo. Rubeni alipoteza pendeleo hilo kwa sababu ya mwenendo wake mpotovu. (1 Nyakati 5:1) Hata hivyo, chini ya Sheria ya Musa, mwanamume aliyekuwa na zaidi ya mke mmoja hangeweza kuchukua faida za haki ya mwana wa kwanza wa mke wa kwanza na kumpa mwana wa kwanza wa mke wa pili eti kwa sababu alimpenda zaidi mke wake wa pili. Baba alipaswa kuheshimu haki ambayo bila shaka ilikuwa ya mzaliwa wake wa kwanza.—Kumbukumbu la Torati 21:15-17.

Kwa nini waandishi na Mafarisayo walivaa “vibweta vyenye maandiko”?

Yesu aliwashutumu maadui wake wa kidini, waandishi na Mafarisayo, kwa sababu walipanua “vibweta vyenye maandiko ambavyo [walivaa] kama ulinzi.” (Mathayo 23:2, 5) Wafuasi wa vikundi hivyo vya kidini walijifunga kwenye vipaji vya nyuso zao vibweta vidogo vyeusi vya ngozi vyenye umbo la pembe-mraba au mstatili (rectangle). Walifunga pia vibweta hivyo upande wa ndani wa mkono, karibu na moyo wao. Waliweka mistari ya Maandiko ndani ya vibweta hivyo. Desturi ya kuvaa vibweta vya maandiko kama hivyo, ambavyo viliitwa tepe, ilitokana na zoea la kufuata kihalisi agizo hili la Mungu kwa Waisraeli: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako . . . Nawe uyafunge kama ishara kwenye mkono wako” na “kama utepe wa kipaji katikati ya macho yako.” (Kumbukumbu la Torati 6:6-8) Haijulikani vizuri desturi ya kuvaa tepe ilianza wakati gani, lakini wasomi wengi wanasema ilianza katika karne ya tatu au ya pili K.W.K.

Yesu alishutumu desturi hiyo kwa sababu mbili. Kwanza, waandishi na Mafarisayo walipanua tepe zao ili kuonyesha watu wengine jinsi walivyokuwa watakatifu. Pili, vikundi hivyo vilifikiri kimakosa kwamba vibweta vyao vya maandiko vilikuwa hirizi, ambazo zingewalinda. Neno la Kigiriki la vibweta hivyo, phylakterion, linatafsiriwa kuwa “kituo cha ulinzi,” “ngome,” au “njia ya ulinzi,” katika vitabu ambavyo havihusiani na Biblia.