Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endeleeni Kutenda Mema

Endeleeni Kutenda Mema

Endeleeni Kutenda Mema

“Endeleeni . . . kutenda mema.”—LUKA 6:35.

1, 2. Kwa nini mara nyingi si rahisi kuwatendea wengine mema?

SI RAHISI kuwatendea wengine mema. Huenda wale ambao tunawaonyesha upendo wasitutendee mema. Ingawa tunafanya yote tunayoweza ili kuwasaidia watu kiroho kwa kuwahubiria “habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha” na Mwana wake, huenda wakawa wenye ubaridi au wasio na shukrani. (1 Tim. 1:11) Wengine wamekuwa ‘adui wenye chuki wa mti wa mateso wa Kristo.’ (Flp. 3:18) Tukiwa Wakristo, tunapaswa kuwatendea jinsi gani?

2 Yesu Kristo aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kutenda mema.” (Luka 6:35) Acheni basi tuchunguze kwa makini himizo hilo. Pia, tutafaidika na mambo mengine ambayo Yesu alisema kuhusu kuwatendea wengine mema.

‘Muwapende Adui Zenu’

3. (a) Kwa maneno yako mwenyewe, eleza kwa ufupi maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:43-45. (b) Ni maoni gani kuhusu Wayahudi na watu wasio Wayahudi yaliyotokezwa na viongozi wa dini ya Kiyahudi wa karne ya kwanza?

3 Katika Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu aliwaambia wasikilizaji wake wawapende adui zao na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa. (Soma Mathayo 5:43-45.) Waliokuwepo katika pindi hiyo walikuwa Wayahudi, ambao waliijua amri hii ya Mungu: “Usilipize kisasi wala usiwe na kinyongo juu ya wana wa watu wako; nawe mpende mwenzako kama wewe mwenyewe.” (Law. 19:18) Viongozi wa dini ya Kiyahudi wa karne ya kwanza waliamini kwamba maneno “wana wa watu wako” na “mwenzako” yaliwahusu tu Wayahudi. Sheria ya Musa iliwataka Waisraeli wajitenge na mataifa mengine, lakini kulingana na maoni yaliyokuwepo wakati huo, watu ambao si Wayahudi walionwa kuwa maadui na kila mmoja wao alipaswa kuchukiwa.

4. Wanafunzi wa Yesu walipaswa kuwatendea adui zao jinsi gani?

4 Kinyume na hilo, Yesu alisema: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.” (Mt. 5:44) Wanafunzi wake walipaswa kuwatendea kwa upendo wale wote ambao waliwachukia. Kulingana na Luka, mwandikaji wa Injili, Yesu alisema hivi: “Mimi ninawaambia ninyi mnaosikiliza, Endeleeni kuwapenda adui zenu, kuwafanyia mema wale wanaowachukia, kuwabariki wale wanaowalaani, kusali kwa ajili ya wale wanaowatusi.” (Luka 6:27, 28) Kama watu wa karne ya kwanza ambao walifuata maneno ya Yesu, ‘tunawafanyia mema wale wanaotuchukia’ kwa kuwatendea kwa fadhili. ‘Tunawabariki wale wanaotulaani’ kwa kuzungumza nao kwa njia ya fadhili. Na ‘tunasali kwa ajili ya wale wanaotutesa’ kimwili au ‘wanaotutusi’ au kututesa kwa njia nyinginezo. Sala hizo zinaonyesha kwamba tunawapenda maadui wetu kwa sababu tunasali ili wabadili mioyo yao na kuchukua hatua ambayo itawaletea kibali cha Yehova.

5, 6. Kwa nini tunapaswa kuwapenda adui zetu?

5 Kwa nini tunapaswa kuwapenda adui zetu? Yesu alisema, “Ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.” (Mt. 5:45) Tunapotii shauri hilo, tunakuwa “wana” wa Mungu kwa kumwiga Yehova, ambaye “hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” Kama simulizi la Luka linavyoonyesha, Mungu “ni mwenye fadhili kuwaelekea wasio na shukrani na waovu.”—Luka 6:35.

6 Akikazia umuhimu wa wanafunzi wake ‘kuendelea kuwapenda adui zao,’ Yesu alisema hivi: “Mkiwapenda wale wanaowapenda ninyi, mna thawabu gani? Je, wakusanya-kodi pia hawafanyi jambo hilohilo? Na mkiwasalimu ndugu zenu tu, mnafanya jambo gani linalozidi lile la kawaida? Je, watu wa mataifa pia hawafanyi jambo hilohilo?” (Mt. 5:46, 47) Ikiwa tungewapenda tu wale wanaotupenda, hilo halingetufanya tustahili “thawabu” yoyote kutoka kwa Mungu, au kupata kibali chake. Hata wakusanya-kodi, ambao walidharauliwa, waliwapenda watu ambao waliwapenda.—Luka 5:30; 7:34.

7. Kwa nini halingekuwa jambo linalozidi lile la kawaida ikiwa tungewasalimu “ndugu” zetu tu?

7 Salamu ya kawaida ya Wayahudi ilitia ndani neno “amani.” (Amu. 19:20; Yoh. 20:19) Kusudi la salamu hiyo lilikuwa kumtakia mtu afya njema, hali njema, na ufanisi. Halingekuwa ‘jambo linalozidi lile la kawaida’ ikiwa tungewasalimu tu wale ambao tunawaona kuwa “ndugu” zetu. Kama Yesu alivyoonyesha, “watu wa mataifa” walifanya vivyo hivyo.

8. Yesu alikuwa akiwatia moyo wasikilizaji wake wafanye nini aliposema: ‘Lazima muwe wakamilifu’?

8 Kwa sababu ya dhambi waliyorithi, wanafunzi wa Kristo hawangekuwa wakamilifu, bila kasoro yoyote. (Rom. 5:12) Hata hivyo, Yesu alimalizia sehemu hiyo ya hotuba yake kwa kusema: “Lazima ninyi basi muwe wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Mt. 5:48) Hivyo, alikuwa akiwatia moyo wasikilizaji wake wamwige Yehova, ‘Baba yao wa mbinguni,’ kwa kuukamilisha upendo wao, yaani, kuufanya uwe kamili kwa kuwapenda maadui wao. Tunatazamiwa tufanye vivyo hivyo.

Kwa Nini Uwe Mwenye Kusamehe?

9. Maneno: “Utusamehe madeni yetu” yanamaanisha nini?

9 Tunaendelea kutenda mema tunapomsamehe kwa rehema mtu anayetutendea dhambi. Sala ya mfano ya Yesu ina maneno haya: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.” (Mt. 6:12) Bila shaka, maneno hayo hayamaanishi kusamehe madeni ya pesa. Injili ya Luka inaonyesha kwamba “madeni” ambayo Yesu alikuwa akizungumzia ni dhambi, kwa kuwa inasema hivi: “Utusamehe dhambi zetu, kwa maana sisi wenyewe pia humsamehe kila mtu aliye na deni letu.”—Luka 11:4.

10. Kuhusu kusamehe, tunaweza kumwiga Mungu jinsi gani?

10 Tunapaswa kumwiga Mungu, ambaye anawasamehe kwa hiari watenda-dhambi wenye kutubu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.” (Efe. 4:32) Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Yehova ni mwenye rehema na mwenye neema, si mwepesi wa hasira na ni mwingi wa fadhili zenye upendo. . . . Hakututendea kulingana na dhambi zetu; wala kuleta juu yetu kile tunachostahili kulingana na makosa yetu. . . . Kama vile mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo ameweka makosa yetu mbali sana na sisi. Kama vile baba anavyowaonyesha wanawe rehema, ndivyo ambavyo Yehova amewaonyesha rehema wale wanaomwogopa. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.”—Zab. 103:8-14.

11. Mungu anawasamehe nani?

11 Watu wanaweza kusamehewa na Mungu ikiwa tu wao wenyewe tayari wamewasamehe wale waliowatendea dhambi. (Marko 11:25) Ili kukazia jambo hilo, Yesu aliongeza hivi: “Kwa maana ikiwa mnawasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi pia; lakini ikiwa hamtawasamehe watu makosa yao, Baba yenu naye hatawasamehe makosa yenu.” (Mt. 6:14, 15) Ndiyo, Mungu anawasamehe wale tu ambao wanawasamehe wengine kutoka moyoni. Na njia moja ya kuendelea kutenda mema ni kufuata shauri hili la Paulo: “Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.”—Kol. 3:13.

“Acheni Kuhukumu”

12. Yesu alitoa shauri gani kuhusu kuwahukumu wengine?

12 Njia nyingine ya kutenda mema ilionyeshwa katika Mahubiri ya Mlimani wakati Yesu alipowaambia wasikilizaji wake waache kuwahukumu wengine kisha akatumia mfano wenye nguvu ili kukazia jambo hilo. (Soma Mathayo 7:1-5.) Acheni tuchunguze kile ambacho Yesu alimaanisha aliposema: “Acheni kuhukumu.”

13. Wasikilizaji wa Yesu walipaswa ‘kuendelea kuachilia’ jinsi gani?

13 Injili ya Mathayo inamnukuu Yesu akisema: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe.” (Mt. 7:1) Kulingana na Luka, Yesu alisema hivi: “Acheni kuhukumu, nanyi hamtahukumiwa; na acheni kulaumu, nanyi hamtalaumiwa. Endeleeni kuachilia, nanyi mtaachiliwa.” (Luka 6:37) Mafarisayo wa karne ya kwanza waliwahukumu wengine kwa ukali, kwa msingi wa mapokeo yasiyo ya Kimaandiko. Wasikilizaji wa Yesu ambao waliwahukumu wengine walipaswa ‘kuacha kuhukumu.’ Badala yake, walipaswa ‘kuendelea kuachilia,’ yaani, kuwasamehe wengine makosa yao. Mtume Paulo alitoa shauri kama hilo kuhusu kusamehe kama ilivyotajwa tayari.

14. Kwa kuwasamehe wengine, wanafunzi wa Yesu wangewachochea watu kufanya nini?

14 Kwa kuwasamehe wengine, wanafunzi wa Yesu wangewachochea watu kuwa wenye kusamehe. Yesu alisema: “Kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa; na kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi.” (Mt. 7:2) Tunavuna kile tunachopanda ikitegemea jinsi tunavyowatendea wengine.—Gal. 6:7.

15. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba ni kosa kuwa mwenye kuchambua-chambua?

15 Kumbuka Yesu alionyesha kwamba ni kosa kuwa mwenye kuchambua-chambua alipouliza hivi: “Basi, kwa nini unautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe? Au unawezaje kumwambia ndugu yako, ‘Niruhusu niutoe unyasi ulio katika jicho lako’; wakati, tazama! boriti limo katika jicho lako mwenyewe?” (Mt. 7:3, 4) Mtu aliye na mwelekeo wa kuchambua-chambua wengine anaona kosa dogo lililo katika “jicho” la ndugu yake. Mchambuaji huyo kwa kweli anafikiri kwamba ndugu yake haelewi mambo vizuri na hana uwezo wa kufanya maamuzi. Ingawa kosa hilo ni dogo kama unyasi, mchambuaji anaomba ‘aondoe unyasi’ huo. Kwa unafiki anajitolea kumsaidia ndugu yake kuona mambo waziwazi zaidi.

16. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mafarisayo walikuwa na “boriti” katika jicho lao?

16 Viongozi wa dini ya Kiyahudi hasa waliwachambua sana wengine. Kwa mfano: Mwanamume mmoja kipofu ambaye aliponywa na Kristo aliposema kwamba lazima Yesu awe alitoka kwa Mungu, Mafarisayo walijibu kwa hasira: “Wewe ulizaliwa katika dhambi, na bado je, wewe unatufundisha sisi?” (Yoh. 9:30-34) Mafarisayo walikuwa na “boriti” katika jicho lao wenyewe na walikuwa vipofu kabisa hivi kwamba hawakuweza kuona mambo kwa njia ya kiroho na kufanya maamuzi kwa njia inayofaa. Kwa hiyo, Yesu alisema hivi: “Mnafiki! Kwanza toa boriti lililo katika jicho lako mwenyewe, na ndipo utakapoona waziwazi jinsi ya kuutoa unyasi ulio katika jicho la ndugu yako.” (Mt. 7:5; Luka 6:42) Tukiazimia kutenda mema na kuwatendea wengine vizuri, hatutawachambua vikali, huku tukitafuta sikuzote unyasi wa mfano katika jicho la ndugu yetu. Badala yake, tutatambua kwamba sisi si wakamilifu na hivyo tunapaswa kuepuka kuwahukumu na kuwachambua-chambua waamini wenzetu.

Jinsi Tunavyopaswa Kuwatendea Wengine

17. Kulingana na Mathayo 7:12, tunapaswa kuwatendea wengine jinsi gani?

17 Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alisema kwamba Mungu anaonyesha mtazamo kama wa baba kuelekea watumishi Wake kwa kujibu sala zao. (Soma Mathayo 7:7-12.) Inapendeza kujua kwamba Yesu aliweka kanuni hii ya mwenendo: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mt. 7:12) Ni kwa kuwatendea wanadamu wenzetu katika njia hiyo tu ndipo tunapothibitisha kwamba sisi ni wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo.

18. “Sheria” ilionyesha jinsi gani kwamba tunapaswa kuwatendea wengine jinsi tunavyotaka watutendee?

18 Baada ya kusema kwamba tunapaswa kuwatendea wengine jinsi tunavyotaka watutendee, Yesu aliongeza hivi: “Hii, kwa kweli, ndiyo maana ya Sheria na Manabii.” Tunapowatendea wengine katika njia ambayo Yesu alisema, tunatenda kulingana na kusudi la “Sheria,” yaani, maandishi yanayofanyiza vitabu vya Biblia kuanzia Mwanzo mpaka Kumbukumbu la Torati. Mbali na kufunua kusudi la Yehova la kutokeza uzao ambao utaondoa uovu, vitabu hivyo vinafafanua Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli kupitia Musa mwaka wa 1513 K.W.K. (Mwa. 3:15) Kati ya mambo mengine, Sheria ilionyesha wazi kwamba Waisraeli walipaswa kuwa wenye haki, wasio na ubaguzi, na walipaswa kuwatendea mema wenye kuteseka na wakaaji wageni katika nchi.—Law. 19:9, 10, 15, 34.

19. “Manabii” wanaonyesha jinsi gani kwamba tunapaswa kutenda mema?

19 Yesu alipotaja “Manabii,” alikuwa akifikiria vitabu vya unabii vya Maandiko ya Kiebrania. Vina unabii mbalimbali kumhusu Masihi ambao Kristo mwenyewe alitimiza. Pia, maandishi hayo yanaonyesha kwamba Mungu anawabariki watu wake wanapotenda yaliyo sawa machoni pake na kuwatendea wengine kwa njia inayofaa. Kwa mfano, unabii wa Isaya ulitoa shauri hili kwa Waisraeli: “Yehova amesema hivi: ‘Shikeni haki, na mfanye yaliyo ya uadilifu. . . . Mwenye furaha ni yule mwanadamu anayeweza kufa ambaye hufanya jambo hili, na mwana wa binadamu anayelishika, . . . kuuzuia mkono wake ili asitende ubaya wa aina yoyote.’” (Isa. 56:1, 2) Ndiyo, Mungu anawatazamia watu wake waendelee kutenda mema.

Sikuzote Watendee Wengine Mema

20, 21. Umati uliitikia jinsi gani Mahubiri ya Yesu ya Mlimani, na kwa nini unapaswa kuyatafakari?

20 Tumechunguza mambo machache tu kati ya mambo mengi ya maana ambayo Yesu alisema katika Mahubiri yake ya Mlimani yasiyo na kifani. Hata hivyo, tunaweza kuelewa kwa urahisi jinsi wale waliosikia maneno yake walivyoitikia wakati huo. Biblia inasema hivi: “Basi wakati Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, umati ukashangazwa na njia yake ya kufundisha; kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka, na si kama waandishi wao.”—Mt. 7:28, 29.

21 Bila shaka, Yesu Kristo alithibitika kuwa “Mshauri wa Ajabu” aliyetabiriwa. (Isa. 9:6) Mahubiri ya Mlimani yanaonyesha kwa njia bora sana kwamba Yesu anajua jinsi Baba yake wa mbinguni anavyoona mambo. Zaidi ya mambo ambayo tumezungumzia, hotuba hiyo ina mambo mengi kuhusu furaha ya kweli, jinsi ya kuepuka upotovu wa maadili, jinsi ya kutenda uadilifu, yale tunayopaswa kufanya ili tupate maisha salama na yenye shangwe wakati ujao, na mengine mengi. Basi, tunakutia moyo usali na kusoma tena kwa makini Mathayo sura ya 5 mpaka 7. Tafakari mashauri mazuri ajabu ya Yesu katika sura hizo. Tumia katika maisha yako yale ambayo Kristo alisema katika Mahubiri yake ya Mlimani. Ukifanya hivyo, utampendeza Yehova zaidi, utawatendea wengine kwa njia inayofaa, na utaendelea kutenda mema.

Ungetoa Jibu Gani?

• Tunapaswa kuwatendea adui zetu jinsi gani?

• Kwa nini tunapaswa kuwa wenye kusamehe?

• Yesu alisema nini kuhusu kuwahukumu watu?

• Kulingana na Mathayo 7:12, tunapaswa kuwatendea wengine jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 10]

Je, unajua kwa nini Yesu alisema: “Acheni kuhukumu”?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kwa nini tunapaswa kusali kwa ajili ya wale wanaotutesa?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je, sikuzote unawatendea wengine jinsi ambavyo ungependa wakutendee?