Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Iweni na Dhamiri Njema”

“Iweni na Dhamiri Njema”

“Iweni na Dhamiri Njema”

WATU wengi huamini kwamba wanapaswa kuongozwa na dhamiri zao wanapofanya maamuzi. Lakini ili dhamiri yetu ituongoze kwa njia yenye kutegemeka, inahitaji kuzoezwa ifaavyo ili kupambanua mema na mabaya, na ni lazima tutii mwongozo wake.

Fikiria kisa cha mwanamume aitwaye Zakayo kama kinavyosimuliwa katika Biblia. Zakayo, aliyeishi Yeriko alikuwa mkusanya-kodi mkuu na tajiri. Alisema kwamba alipata utajiri wake kwa unyang’anyi—zoea ambalo bila shaka liliwaumiza wengine. Je, dhamiri ya Zakayo ilimsumbua kwa sababu ya matendo yake yasiyo ya haki? Ikiwa ilimsumbua, basi yaonekana alikuwa akiipuuza.—Luka 19:1-7.

Hata hivyo, hali fulani ilitokea ambayo ilimfanya Zakayo afikirie tena mwenendo wake. Yesu alikuja Yeriko. Zakayo aliyekuwa mfupi alitaka kumwona Yesu, lakini hangeweza kwa sababu ya umati. Kwa hiyo, alikimbia mbele yao na kupanda juu ya mti ili aweze kumwona vizuri. Yesu alivutiwa na jinsi Zakayo alivyotamani sana kumwona na akamwambia kwamba angemtembelea nyumbani kwake. Zakayo alimkaribisha kwa furaha mgeni wake mheshimiwa.

Zakayo aliguswa moyo na yale aliyosikia na kuona alipokuwa na Yesu, nayo yalimchochea kubadili mwenendo wake. Alisema hivi: “Tazama! Nusu ya mali zangu, Bwana, mimi ninawapa maskini, na chochote kile nilichonyang’anya yeyote kwa shtaka lisilo la kweli ninarudisha mara nne.”—Luka 19:8.

Dhamiri ya Zakayo iliamshwa, akaisikiliza na kuitii. Alinufaika sana. Wazia jinsi Zakayo alivyohisi Yesu alipomwambia hivi: “Siku hii wokovu umekuja kwenye nyumba hii!”—Luka 19:9.

Huo ni mfano wenye kutia moyo kama nini! Unaonyesha kwamba tunaweza kubadili mwenendo wowote ule tuliokuwa nao hapo awali. Kama Zakayo, tunaweza kutii maneno ya Yesu yaliyo katika Biblia na kusitawisha uwezo wa kupambanua mema na mabaya. Kisha tunaweza ‘kuwa na dhamiri njema’ kama mtume Petro alivyohimiza. Tunaweza kuitii dhamiri yetu iliyozoezwa na kufanya yaliyo mema.—1 Petro 3:16.