Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Ubaya Wowote Kutaka Kuwa na Faragha?

Je, Kuna Ubaya Wowote Kutaka Kuwa na Faragha?

Vijana Huuliza

Je, Kuna Ubaya Wowote Kutaka Kuwa na Faragha?

Weka ✔ kando ya jibu ambalo huenda ukachagua katika kila moja ya hali zifuatazo.

1. Uko ndani ya chumba chako cha kulala kisha ndugu au dada yako anaingia bila kubisha.

‘Ni sawa tu . . . mimi hufanya hivyo pia.’

‘Huo ni utovu wa adabu! Namna gani ikiwa ningekuwa ninavaa?’

2. Unazungumza na rafiki kwenye simu, na mama yako anasikiliza kila kitu unachosema.

‘Ni sawa tu . . . sina la kuficha.’

‘Haifai! Ninahisi ni kama ninachunguzwa!’

3. Umerudi tu nyumbani na wazazi wote wanaanza kukurushia maswali. “Ulikuwa wapi? Ulikuwa ukifanya nini? Ulikuwa na nani?”

‘Ni sawa tu . . . mimi huwaambia kila kitu.’

‘Inaudhi sana! Wazazi wangu hawaniamini!’

HUENDA ulipokuwa kijana faragha haikuwa jambo kubwa sana. Wakati ndugu na dada zako wadogo walipoingia chumbani mwako ghafla, uliwakaribisha bila kulalamika. Wazazi wako walipokuuliza swali lolote, uliwajibu bila kusitasita. Kila mtu alijua kilichokuwa kikiendelea maishani mwako. Lakini huenda sasa unatamani kuwa na faragha. “Mimi hufurahi ninapoweza kuficha mambo fulani,” anasema Corey mwenye miaka 14. *

Kwa nini sasa unatamani kuwa na faragha? Huenda ikawa ni kwa sababu unakua. Kwa mfano, huenda mabadiliko yanayotokea katika mwili wako wakati wa kubalehe yakakufanya usijihisi ukiwa huru, hata unapokuwa mbele ya watu wa familia yako. Pia unapoendelea kukua, unaanza kuhisi unataka kujifanyia maamuzi yako mwenyewe. Hiyo inaonyesha kwamba umeanza kuwa na “uwezo wa kufikiri”—sifa ambayo Biblia huonyesha kuwa vijana wanapaswa kuwa nayo. (Methali 1:1, 4; Kumbukumbu la Torati 32:29) Hata Yesu alienda “mahali pasipo na watu” ili atafakari.—Mathayo 14:13.

Bila shaka, bado uko chini ya wazazi wako, na wana haki ya kujua kinachoendelea maishani mwako. (Waefeso 6:1) Lakini huenda kuwe na kutoelewana kwa sababu wazazi wako wanataka kujua kinachoendelea na wewe unahisi kwamba unataka kuwa na faragha zaidi. Unaweza kukabiliana jinsi gani na hali hiyo? Wacha tuchanganue sehemu mbili ambazo huenda matatizo yakatokea.

Unapojaribu Kuwa Peke Yako

Kuna sababu kadhaa zinazofanya utake kuwa peke yako. Huenda ikawa unataka ‘kupumzika kidogo.’ (Marko 6:31) Au unapotaka kusali, unaweza kufanya kama Yesu alivyowashauri wanafunzi wake, “ingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako.” (Mathayo 6:6; Marko 1:35) Tatizo ni kuwa, unapofunga mlango wa chumba chako cha faragha (ikiwa unacho), huenda wazazi wako wasijue kuwa unasali! Na ndugu na dada zako hawataelewa ni wakati gani unapotaka kuwa peke yako.

Unachoweza kufanya. Badala ya kugombana na watu wengine wa familia yako, fanya mambo yafuatayo.

● Jaribu kuwawekea ndugu na dada zako sheria fulani zenye usawaziko ili uwe na wakati wa kuwa peke yako. Ikiwa ni lazima, waombe wazazi wako wakusaidie katika jambo hilo.

● Jaribu kuelewa maoni ya wazazi wako. “Wakati fulani wazazi wangu hutaka kujua ninaendeleaje,” anasema Rebekah mwenye umri wa miaka 16. “Lakini kusema kweli ikiwa ningekuwa mzazi, ningetaka kujua kijana wangu yuko katika hali gani hasa wakati huu ambao vijana wanakabili majaribu ya kila aina!” Kama Rebekah, je, unaweza kuelewa kwa nini wazazi wako wanakujali?—Methali 19:11.

● Jiulize hivi kwa unyoofu: ‘Je, ninafanya wazazi wangu washuku kuwa kuna jambo baya ninalotaka kufanya ninapofunga mlango wa chumba changu? Je, nimekuwa nikificha mambo mengi kuhusu maisha yangu hadi wanahisi kuwa wanahitaji kutumia mbinu za ukachero ili wanifahamu?’ Kwa kweli, unavyozidi kuwa wazi kwa wazazi wako, ndivyo watakavyozidi kukuamini. *

Mikakati. Andika hapa chini kile unachoweza kusema ili kuanzisha mazungumzo na wazazi wako kuhusu jambo hili.

․․․․․

Unapotafuta marafiki

Unapobalehe, ni jambo la kawaida kutafuta marafiki ambao si watu wa familia yako. Pia, ni jambo la kawaida kwa wazazi wako kutaka kujua rafiki zako na kile mnachofanya pamoja. Kwa wazazi wako, hiyo ni sehemu ya kazi yao, yaani, ni jambo ambalo wanajua wanapaswa kufanya. Hata hivyo, huenda ukafikiri kwamba wazazi wako wanakushuku. “Nataka tu kutumia simu yangu ya mkononi na kutuma barua pepe bila wazazi wangu kuniuliza kila wakati ninazungumza na nani,” anasema Amy mwenye umri wa miaka 16.

Unachoweza kufanya. Badala ya kuruhusu urafiki wako na watu wengine uharibu uhusiano wako na wazazi wako, jaribu kufanya mambo yafuatayo.

● Hakikisha kuwa wazazi wako wanawafahamu vizuri rafiki zako. Bila shaka, hungependa wazazi wako watumie mbinu za kikachero kuwafahamu rafiki zako, lakini ikiwa hutaki wawajue huenda wakalazimika kufanya hivyo. Kumbuka kuwa wazazi wako wanatambua kuwa rafiki zako wanaweza kukuathiri sana. (1 Wakorintho 15:33) Wanavyozidi kuwajua watu unaoshirikiana nao ndivyo watakavyozidi kukuruhusu ujichagulie rafiki zako.

● Kwa heshima waeleze wazazi wako kuhusu jambo hilo. Usiwashutumu eti wanaingilia mambo yasiyowahusu. Badala ya hivyo unaweza kusema, “Mimi huhisi kuwa kila kitu ninachozungumza na rafiki zangu lazima kichunguzwe. Na hivyo ni vigumu kwangu kuzungumza nao.” Huenda wazazi wako wakakupa uhuru zaidi wa kuzungumza na rafiki zako.—Methali 16:23.

● Jichunguze kwa unyoofu: Je, jambo ambalo hasa unatafuta ni kupata faragha au kuficha mambo? Brittany mwenye umri wa miaka 22, anasema hivi: “Ikiwa unaishi nyumbani na wazazi wako wanakujali sana, kila wakati unapaswa kuwa ukijiambia hivi, ‘Ikiwa kile ninachofanya si kosa, kwa nini nijifiche?’ Ikiwa ni lazima ufiche unachofanya basi huenda jambo hili si sawa.”

Mikakati. Andika hapa chini kile unachoweza kusema ili kuanzisha mazungumzo na wazazi wako kuhusu jambo hili.

․․․․․

Jinsi ya Kupata Faragha

Sasa fikiria jinsi unavyoweza kupata faragha.

Hatua ya 1: Tambua tatizo.

Ni katika maeneo yapi unayohisi unataka kuwa na faragha?

․․․․․

Hatua ya 2: Fikiria sababu za wazazi wako.

Unafikiri huenda wazazi wako wanahangaikia nini hasa?

․․․․․

Hatua ya 3: Tafuta suluhisho.

(a) Fikiria angalau njia moja ambayo unaweza kuchangia tatizo hilo, na uiandike hapa chini.

․․․․․

(b) Kupatana na jibu lako hapo juu, unaweza kufanya marekebisho gani?

․․․․․

(c) Ungependa wazazi wako washughulikie jinsi gani matatizo yako?

․․․․․

Hatua ya 4: Zungumza na wazazi wako.

Zungumzia kile ambacho umeandika hapa juu pamoja na wazazi wako wakati unaofaa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 21 Ikiwa wazazi wako wanaonekana kuwa hawakuamini, kwa upole na heshima waeleze jinsi unavyohisi. Sikiliza kwa makini sababu zao, na uhakikishe kuwa haufanyi jambo lolote linalochangia tatizo hilo.—Yakobo 1:19.

MAMBO YA KUFIKIRIA

● Kwa nini wazazi wako wana haki ya kutaka kujua kuhusu maisha yako?

● Jitihada za kusitawisha mbinu za kuwasiliana na wazazi wako, zitakusaidia jinsi gani baadaye maishani kuwasiliana na watu wengine?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Vijana wasipowaficha wazazi wao chochote, basi wazazi hawatakuwa na sababu za kusoma barua-pepe na ujumbe mfupi wa vijana wao ili wajue kinachoendelea.”

“Siwezi kukasirika ikiwa wazazi watasoma barua-pepe nilizotumiwa. Ikiwa mwajiri ana haki ya kusoma barua-pepe za wafanyakazi wake, kwa nini wazazi wasisome barua-pepe za watoto wao?”

“Wazazi hawataki upatwe na jambo lolote baya, na nyakati nyingine huenda ikaonekana ni kama wanaingilia mambo yako ya kibinafsi. Huenda hilo lisionekane kuwa sawa. Lakini, kusema kweli, huenda ningefanya vivyo hivyo ikiwa ningekuwa mzazi.”

[Picha]

Eden

Kevin

Alana

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

TAARIFA KWA WAZAZI

● Mwana wako yuko ndani ya chumba chake cha kulala. Je, uingie bila kubisha?

● Binti yako amesahau simu yake ya mkononi alipokuwa akiharakisha kwenda shuleni. Je, uanze kuchunguza ujumbe aliotumiwa?

Hayo si maswali rahisi kujibu. Kwa upande mmoja, una haki ya kujua kile ambacho kijana wako anafanya na una jukumu la kumlinda. Kwa upande ule mwingine, huwezi kuwa kachero, ukichunguza kila kitu anachofanya. Kwa hiyo, unaweza kuwa na usawaziko jinsi gani?

Kwanza, tambua kwamba kijana wako anapotafuta kuwa na faragha haimaanishi kwamba anafanya jambo lolote baya. Ni kawaida kwa vijana kufanya hivyo wanapokua. Kuwa na faragha huwazoeza vijana kuwa na uwezo wa kujitafutia marafiki na kujitatulia shida zao kwa kutumia ‘nguvu zao za kufikiri.’ (Waroma 12:1, 2) Kuwa na faragha pia huwasaidia kukuza uwezo wa kufikiri. Hiyo ni sifa muhimu itakayowawezesha kutenda kama watu waliokomaa. (1 Wakorintho 13:11) Pia inawapa nafasi ya kutafakari kabla ya kujibu maswali magumu.—Methali 15:28.

Pili, tambua kwamba unapojaribu kuongoza kila sehemu ya maisha ya kijana wako utamfanya tu akuchukie na aasi. (Waefeso 6:4; Wakolosai 3:21) Je, hilo linamaanisha kwamba unapaswa kumwacha afanye anachotaka? Hapana, kwa kuwa bado wewe ndiye mzazi wake. Hata hivyo, lengo lako ni kumsaidia mtoto wako awe na dhamiri iliyozoezwa. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Methali 22:6) Kwa hiyo, ni afadhali kumwongoza kijana kuliko kumchunga.

Tatu, zungumzia jambo hilo pamoja na kijana wako. Sikiliza maoni yake. Je, kuna wakati unapoweza kukubali sababu zake? (Wafilipi 4:5) Mwache kijana wako ajue kwamba utamruhusu kuwa na faragha kwa kiasi fulani iwapo tu atadumisha uaminifu wake. Taja waziwazi adhabu atakayopata kwa kutotii, na uhakikishe kwamba unaitoa inapohitajika. Uwe na hakika kwamba unaweza kumpa kijana wako faragha yake bila kutupilia mbali jukumu lako la kuwa mzazi mwenye kujali.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Uaminifu ni kama mshahara—lazima uufanyie kazi ili uupate